Wednesday, November 2, 2016

IDADI YA WATUMISHI HEWA KUFIKIA 19,629.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki
                                              ANGELINA KAIRUKI.
Watumishi hewa 19,629 wamebainika kuwapo nchini tangu uhakiki ufanyike; na kama wangelipwa, serikali ingepoteza Sh bilioni 19.7 kwa mwezi.
Aidha, kutokana na hali hiyo, serikali imechukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi 1,663 kutoka katika taasisi zake kwa watumishi waliohusika na kuwepo kwa watumishi hewa na kati ya hizo, watumishi 638 wamefunguliwa mashtaka polisi.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki, alisema bungeni mjini hapa jana kuwa serikali ingepata hasara hiyo, endapo watumishi hao hewa wangelipwa kwa mwezi.
Akitoa mfano wa halmashauri mbili, Kairuki alisema Kinondoni imekutwa na watumishi hewa 107 na kama wangelipwa ingepoteza Sh bilioni 1.279 na kwa Halmashauri ya Kishapu waligundulika 73 na wangelipwa Sh milioni 543.
Kairuki alikuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Maida Hamad Abdallah (CCM) aliyetaka kujua hasara serikali imeipata kwa kuwalipa watumishi hewa na adhabu kwa waliohusika na suala hilo.
Alisema, “Hadi sasa watumishi hewa 19,629 wamebainika na kama wangelipwa, kwa mwezi wangeingiza hasara ya Sh 19,749,737,180. Kuhusu adhabu na kurejesha fedha, Kairuki alisema mahakama imekuwa ikitekeleza majukumu yake na kuwatoza faini na wengine kutakiwa kurejesha fedha.
Awali, akijibu swali la msingi la Abdallah aliyetaka kujua serikali inasema nini juu ya wale wote waliohusika kurudisha nyuma maendeleo ya nchi kwa njia hiyo ya watumishi hewa, huku waliohusika wengi wakiwa ni maofisa na watumishi wa serikali, Kairuki alisema hadi Oktoba 25 mwaka huu serikali imechukua hatua za kinidhamu dhidi ya watumishi 1,663.
Kairuki alisema watumishi hao ni kutoka katika wizara, idara zinazojitegemea, wakala wa serikali, sekretarieti za mikoa na mamlaka za serikali za mitaa ambao walibainika kusababisha kuwepo kwa watumishi hewa na 638 kati yao wamefunguliwa mashitaka polisi.
Akitoa mchanganuo, Kairuki alisema idadi ya watumishi waliochukuliwa hatua za kinidhamu katika wizara ni 16, idara zinazojitegemea na Wakala wa Serikali ni tisa, Sekretarieti za mikoa sita na Mamlaka ya Serikali za Mitaa 1,632 wanaofanya idadi ya watumishi 1,663 waliochukuliwa hatua.
“Hatua hii inajumuisha kuwasilishwa kwa masuala yanayowahusu baadhi ya watumishi hawa katika vyombo na ulinzi na usalama na hadi kufikia tarehe 25.10.2016, watumishi 638 mashitaka yako polisi, 50 wanafanyiwa uchunguzi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na watumishi 975 mashtaka yao yamefikishwa kwenye mamlaka zao za kinidhamu,” alisema Kairuki.
Alisema sambamba na hatua hiyo, serikali inaendesha ukaguzi wa mara kwa mara wa Mfumo wa Taarifa za Kiutumishi (HCMIS) na maofisa wanaobainika kuhusika au kusababisha kuwepo kwa watumishi hewa katika taasisi na mamlaka zao, huchukuliwa hatua za kinidhamu, kama vile kuwafungia dhamana na uwezo wa kuingia na kufanya kazi katika mfumo huo.

NAPE AWAPA MAKAVU YANGA.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye.
  WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO, NAPE NNAUYE.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye amesema kuwa Yanga haikufuata taratibu katika mchakato wake wa kubadili umiliki kwani hata Mkutano Mkuu wa wanachama uliendeshwa kienyeji.
Mbali na hilo, Nape pia alisema kuwa kabla ya kuhitimisha mkutano huo wa wanachama, uongozi wa Yanga ulitakiwa kutoa notisi ya siku 60 kwa wanachama wake kama Katiba yao inavyoagiza.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka Dodoma katika kipindi cha radio moja, Nape alisema kuwa Serikali inajua kuwa Manji hafanyi kazi na wajumbe wa Kamati ya Utendaji. Alisema pamoja na kupitwa na wakati kwa sera ya michezo, lakini wadau wamekuwa wakisuasua kutoa mapendekezo ya marekebisho yake ili iweze kuendana na wakati.
“Mkutano ulioitishwa kwanza hakufuata taratibu, walitakiwa kutoa notisi ya siku 60 kwa wanachama wake, lakini hawakufanya hivyo, Serikali tunajua Manji hafanyi kazi na wajumbe wake wa Kamati ya Utendaji,”alisema.
Alisema kuwa sera ya michezo ina mapungufu yanayotakiwa kufanyiwa marekebisho ili kuondoa manung’uniko kwa washika dau, ambao ni klabu za michezo na wanamichezo ambao kwa kipindi kirefu wamekuwa wakilalamikia sera ya michezo kupitwa na wakati.
Wadau hao hususani wa soka wamekuwa wakilitupia lawama Baraza la Michezo la Taifa (BMT), kuwa ni mzigo kwani imekuwa ikipata mgao kwa kila mchezo wa ligi wa asilimia tano ya mapato, huku likiwa halitoi msaada kwa timu za taifa zaidi ya kukabidhi bendera pindi zinapoenda kwenye michuano ya kimataifa.
Hatahivyo, akizungumzia hilo, Nape alisema, “Mapungufu kwenye baraza yapo lakini hayaondoi umuhimu wa baraza kuwepo kwa sasa kwa vile ndio wanaosajili na kusimamia masuala yote ya michezo, kuna mambo mengi mazuri yanayofanywa na baraza na si kweli kuwa halifai kwa kile kitu.” “BMT imekuwa ikifanya mambo mazuri, inawezekana mtu ambaye hajahitaji huduma ya baraza hawezi kujua umuhimu wake, dunia inabadilika sioni shida kufanya mabadiliko lakini sio kulitupia mawe baraza,”alisema.
Kauli ya Nape imekuwa ikiwa ni siku chache baada ya BMT kuzuia klabu za Simba na Yanga kuendelea na mchakato wake wa mabadiliko ya umiliki hadi pale zitakapobadili katiba zake.
Kwa upande wa katibu mkuu wa zamani wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Angetile Osiah alisema sera ya baraza ya mwaka 71 haliendani kwa matakwa ya sasa kwa yanayoendelea ndani ya klabu za michezo.
“Soka letu la kulipwa, ngumi za kulipwa, mpira wa miguu Fifa imetoa maelekezo na katiba za mfano kwa wanachama wake na haitambui baraza kama chombo cha maamuzi ya juu. Licha ya Fifa kuitambua serikali lakini haipi kipaumbele kwenye maamuzi baraza likae chini liangalie nafasi yake kama litaendelea na majukmu yale yale au yabadilishwe,”alisema Osiah.
Hata hivyo, aliwataka watendaji wa Baraza kukaa chini na kujitafakari iwapo nguvu wanayotumia kwa wakati huu bado wanastahili kwani kuzuia mchakato wa mabadiliko kwenye klabu za Simba na Yanga si sahihi.
Wakati Osiah akisema hayo, Mwenyekiti wa zamani wa Simba na ambaye ia amewahi kuwa katibu mkuu wa FAT (sasa TFF), Ismail Aden Rage alisema “BMT ipo sahihi na ina umuhimu mkubwa na kuzitaka klabu za michezo hususani Simba na Yanga kuheshimu maamuzi ya baraza hilo.
“Kusipokuwa na chombo cha juu kama BMT kusimamia michezo itakuwa vurugu mechi kwenye nchi yetu na inaweza kutugawa, mfano mtu anaweza kuanzisha timu yake ya Wanyamwezi Football klabu akasema wanaocheza ni Wanyamwezi tu, hiyo ni hatari lakini baraza halina udini hivyo bado lina umuhimu mkubwa,”alisema.

VYUO VIKUU 15 MATATANI.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Maimuna Tarishi
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Maimuna Tarishi
Serikali imetoa siku mbili kwa vyuo vikuu 15, kuwasilisha matokeo ya mitihani kwa mwaka wa masomo 2015/2016 ya wanafunzi wanufaika na mikopo wanaoendelea na masomo ili kupangiwa mikopo kwa mwaka wa 2016/2017.
Vyuo hivyo vilivyokuwa viwasilishe matokeo hayo siku 30 kabla ya kufunguliwa, vimepewa siku hizo kuanzia jana, kabla serikali haijachukua hatua zozote.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Maimuna Tarishi alisema hayo jana, alipotembelea ofisi za Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu.
Alisema serikali iko katika hatua za mwisho za upangaji na utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wanaoendelea na masomo.
Tarishi alisema baadhi ya vyuo vimeshindwa kuwasilisha matokeo ya mitihani kwa wanafunzi wanaoendelea ili wapangiwe mikopo kwa mwaka unaoendelea, kwani utaratibu lazima vyuo kuwasilisha matokeo kuonesha wanafunzi wangapi wana sifa za kuendelea kupewa mikopo.
“Mikopo haiwezi kutolewa tu kwa kila mwanafunzi, hata kama ameamua kuacha masomo, hivyo vyuo vina wajibu wa kuthibitisha kuwa wanafunzi wanaowaleta bado ni wanafunzi sahihi na wanaendelea na masomo,” alisema Katibu Mkuu huyo.
Alivitaja vyuo ambavyo havijawasilisha matokeo hayo kuwa ni Vyuo vya Elimu ya Biashara (CBE) Dar es Salaam, Mwanza na Dodoma, Chuo Kikuu cha Bagamoyo (UOB), Chuo Kikuu cha St. John Kituo cha St Mark Dar es Salaam (SJUTDSM), Chuo cha St. John Tanzania (SJUT) na Chuo Kikuu cha Tumaini Mbeya (TUMAMBEYA).
Vingine ni Chuo cha Maendeleo ya Jamii (CDTI), Chuo cha United African University of Tanzania (UAUT), Chuo Kikuu cha Teofilo Kisanji (TEKU), Chuo Kikuu Cha Kumbukumbu ya Hubert Kairuki (HKMU), Chuo Kikuu cha Mtakatifu Joseph cha Tiba ya Sayansi (STJCAHS), Chuo Kikuu cha Mtakatifu Joseph Kituo cha Makambako na Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU).
Katibu Mkuu huyo pia alitaka vyuo hivyo kuimarisha mifumo yao ya kuandaa na kuwasilisha matokeo ya mitihani kwa wakati na kwa ukamilifu katika siku zijazo ili kuondoa usumbufu. Akizungumzia hatua watakazochukua wasipotimiza agizo hilo, alisema wanawaagiza kutekeleza maagizo hayo kwa siku walizopewa.
Alisema ana uhakika kauli hiyo inawatosha waungwana hao, kutimiza wajibu wao.
Awali vyuo vyote vya elimu ya juu, vilikumbushwa umuhimu wa kuwasilisha matokeo, kabla havijafunguliwa, ikiwemo serikali kufanya mkutano na Makamu Wakuu wa vyuo vyote vya elimu ya juu mkoani Dodoma na kusisitiza umuhimu wa vyuo kuwasilisha matokeo na nyaraka nyingine muhimu, kabla ya vyuo kufunguliwa.
Alisema Serikali ya Awamu ya Tano, imejipanga kikamilifu na imetenga fedha za kutosha na tayari imetoa Sh bilioni 80.89 kwa ajili ya mikopo ya wanafunzi, wanaonufaika na mikopo hiyo kwa robo ya kwanza ya mwaka.
Alisema kati ya kiasi hicho, tayari Sh bilioni 45.2 zimekwishalipwa na kiasi kilichosalia, kitalipwa kwa vyuo baada ya kupokea matokeo kikamilifu. Pia aliwatoa wasiwasi wanafunzi wa mwaka wa kwanza waliokosa mikopo, kupeleka malalamiko katika dirisha maalum la malalamiko, lililofunguliwa na Bodi ya Mikopo kuanzia juzi na serikali ni sikivu, itafanyia kazi.
Katika siku za hivi karibuni, wanafunzi wa elimu ya juu katika vyuo mbalimbali wanaoendelea na masomo, wamekuwa wakilalamika kucheleweshwa kwa mikopo ya elimu ya juu ; huku wanaoanza mwaka wa kwanza, wakilalamikia kukosa mikopo hiyo.
Imeelezwa kuwa baada ya kufanyika uchambuzi, wanafunzi 20,183 wanaoanza mwaka wa kwanza katika vyuo mbalimbali wamepatiwa mikopo; huku wakitarajia kutoa mikopo kwa wanafunzi 93,295 wanaoendelea na masomo.
Katika hatua nyingine, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Kazi, Vijana na Walemavu, Jenista Mhagama amesema serikali kwa sasa inaandaa taarifa kuhusu mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu; na ikishakamilika itawasilisha bungeni, kama walivyoomba wabunge.
Alitoa ufafanuzi huo baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Najma Giga kujibu mwongozo uliotolewa na Mbunge wa Mwibara, Kange Lugola (CCM) kuomba mwongozo bungeni, akitaka leo serikali ilete taarifa kuhusu mikopo inayotolewa na Bodi ya Mikopo, kwa kile alichoeleza kuwa wanafunzi wengi walioomba mikopo wakiwa na vigezo, hawajapata. Jenista alisema kwa sasa serikali inaandaa taarifa hiyo na ikikamilika, italetwa bungeni kama wabunge walivyoomba.
Akiwasilisha Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na serikali pamoja na mwongozo wa kuandaa mpango na bajeti ya serikali kwa mwaka wa fedha 2017/18, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango alisema Serikali itadhibiti utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu, kwa kuhakikisha kuwa wanafunzi waliokidhi vigezo pekee, ndio wananufaika kwa mikopo hiyo.
Awali, Mhagama alisema serikali haifanyi kazi kwa miujiza, bali kwa kutumia mgangilio wa bajeti iliyowekwa na uthibitisho kwamba serikali inafanya kazi kwa mipango, imeweza kutekeleza kutoa elimu bure ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM.
Mhagama alitoa kauli hiyo baada ya Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Hai, Free Mbowe (Chadema) kuuliza swali la nyongeza lililotokana na swali la msingi la Mbunge wa Shinyanga Mjini, Stephen Masele (CCM) kutaka kujua Serikali itaanza kutekeleza lini ahadi ya Sh milioni 50 kwa kila kijiji na mtaa ili kutatua tatizo la ajira na mitaji kwa vijana na akina mama.
Akifafanua zaidi, alisema kamwe serikali haijiendeshi kwa miujiza bali kwa kutumia mipango iliyojiwekea katika bajeti zake.
“Kuthibitisha jambo hili linatekelezeka, Serikali ya CCM kupitia Ilani yake tumeweza kutoa elimu bure, kuwashangaza Watanzania miradi mikubwa mbalimbali imetekelezwa ikiwemo kununua ndege (mbili za Dash 8, Q400 zilizotengenezwa na Bombardier), Ilani inatekelezwa kwa mambo mengi mbalimbali,” alisema akimjibu swali la nyongeza Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe (Chadema) kuhusu Sh milioni 50 zilizoahidiwa kwa kila kijiji nchini.
Jenista alisema fedha zote zinazoahidiwa na serikali zikiwemo Sh milioni 50, zitatolewa na Watanzania watazipata.
Imeandikwa na Gloria Tesha, Dodoma na Theopista Nsanzugwanko, Dar.

ARSENAL WAPANDA KWENYE CHATI.

Mesut OzilMesut Ozil alifunga bao la dakika za mwisho na kuwawezesha Arsenal kutoka nyuma 2-0 na kulaza Ludogorets Razgrad ya Bulgaria na kuwafikisha hatua ya mondoano Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya.
Ozil alionekana kutulia alipokimbia langoni, akampiga chenga kipa na mabeki wawili na kisha akatumbukiza mpira kimiani.
Awali, matumaini ya Arsenal kurudia ushindi wao mkubwa wa 6-0 mechi ya kwanza yalizimwa Jonathan Cafu alipowaweka Ludogorets mbele baada ya frikiki ya Wanderson.
Cafu alisaidia ufungaji wa pili alipomzidi ujanja Kieran Gibbs na kumpa mpira Claudiu Keseru aliyefunga na kuwashangaza Arsenal.
Granit Xhaka aliokoa jahazi upande wa Arsenal kwa kombora la kutoka hatua 15 kutoka kwa goli baada ya kupokea krosi kutoka Ozil na kufufua matumaini ya Arsenal kwa bao moja.
Olivier Giroud naye alifunga kwa kichwa kutoka kwa mpira uliotoka kwa Aaron Ramsey na kusawazisha.
Kipa wa Arsenal David Ospina alifanya kazi ya ziada kuokoa mpira mara mbili kutoka kwa Wanderson kabla ya Ozil kufunga.
Arsenal sasa wamefika hatua ya 16 bora na wameendeleza msururu wao wa kutoshindwa hadi mechi 15.
Group A

MATOKEO Kamili: Mechi za Ligi ya Mabingwa Ulaya

KUNDI A
Basel 1-2 Paris Saint Germain
Ludo Razgd 2-3 Arsenal
KUNDI B
Besiktas 1-1 Napoli
Benfica 1-0 Dynamo Kiev
KUNDI C
Bor Monchengladbach 1-1 Celtic
Manchester City 3-1 Barcelona
KUNDI D
Atletico Madrid 2-1 FC Rostov
PSV Eindhoven 1-2 Bayern Munich
Mesut Ozil

WALIOHUSIKA NA KIFO CHA MASHALI WASAKWA.



Wakati mwili wa bondia Thomas Mashali ukitarajiwa kuzikwa leo, watu wanne wanasakwa na polisi wakituhumiwa  kuhusika na kifo chake.
Ndugu wa Mashali, Emmanuel Mashali akiwa nyumbani kwao, Tandale kwa Mtogole, Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam alisema kwamba ndugu yao ataagwa leo saa 7:00 mchana na  kuzikwa jioni kwenye makaburi ya Kinondoni.
“Tunajaribu kuomba kutumia Viwanja vya Leaders Club kufanya shughuli za kuaga, kama itashindika shughuli hiyo itafanyika kwenye Viwanja vya Shule ya Msingi Tandale,” alisema Emmanuel na kuongeza: “Shughuli ya kuaga mwili itaanza saa 7:00 mchana na saa 10:00 jioni tutamuhifadhi ndugu yetu kwenye makaburi ya Kinondoni.”
Akizungumzia kifo  hicho, Emmanuel alisema taarifa za awali walizopata ni kwamba bondia huyo alipigwa na watu kadhaa baada ya kumpigia yowe za mwizi.

MBUNGE AKAMATWA NA BUNDUKI 11.



 Kikosi kazi maalumu kilichoundwa na Serikali kupambana na tatizo sugu la ujangili, kimenasa bunduki 11 ambazo zinasadikiwa kutumika kufanya ujangili na kukamata watu wanne zaidi.
Taarifa zilizopatikana jana zimelidokezea gazeti hili kuwa bunduki hizo zilikamatwa nyumbani kwa mbunge wa CCM (jina tunalihifadhi) ambaye bado anasakwa na kikosi kazi hicho.
Matukio hayo yamekuja siku chache baada ya Rais John Magufuli kutaja jina la mtu anayeitwa Mpemba kuhusika na ujangili kwa muda mrefu wakati alipotembelea ofisi za Wizara ya Maliasili na Utalii na kushuhudia pembe 50 za ndovu zilizokamatwa na watumishi wa wizara hiyo.
Siku hiyo, Rais aliwaambia watu aliowaita “vijana” waendelee na kazi yao ya kukamata wauaji wa tembo, akiwahakikishia kuwa Serikali ipo na kuwataka wasiogope mtu yeyote yule.

LADY JAY DEE KIZIMBANI.

Mahakama ya Wilaya Kinondoni imemtia hatiani mwanamuziki nyota wa kike nchini Judith Wambura (Lady Jay Dee) kwa kutoa maneno ya kashfa dhidi ya Joseph Kusaga na Ruge Mutahaba.
Mahakama hiyo imemuamuru aombe radhi kupitia kwenye chombo cha habari chenye "coverage" pana nchini kote na ikiwezekana duniani.
Katika hati ya madai hayo, mwanamuziki huyo anashtakiwa na viongozi wa Clouds Media Group ambao ni Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga kwa kuuchafua uongozi wa kampuni hiyo na viongozi wake kupitia mitandao ya kijamii katika malumbano makali kati ya pande hizo mbili.
Mei 2013, Clouds Media Group na Ruge walimburuza Jay Dee mahakamani kwa kile walichodai kwamba alikuwa akiwatukana kwenye mitandao ya kijamii.