Thursday, November 24, 2016

POLISI MBARONI KWA KUMVUA NGUO MCHUNGAJI NA KUMPIGA PICHA ZA UTUPU.


Polisi wanne wametiwa mbaroni mkoani Kilimanjaro kwa tuhuma za kumvua nguo mchungaji mmoja na kumpiga picha za utupu na mtu mwingine ili wamtuhumu kwamba anafanya mapenzi ya jinsia moja.
Katika mkasa huo uliotokea ndani ya chumba cha hoteli moja wilayani Hai, polisi hao wanaidaiwa kumpiga picha na kisha kumtaka atoe Sh10 milioni ili kumaliza suala hilo. Alitoa Sh5.4 milioni na kuachiwa huru.
Ilivyokuwa
Katika tukio hilo linaloaminika kuwa lilitengenezwa na polisi hao kwa lengo la kujipatia fedha kutoka kwa mchungaji huyo ambaye jina lake na kanisa analohudumu tunalihifadhi kwa sasa, baada ya kuwakuta wawili hao ndani ya chumba, waliwaamuru wavue nguo wakiwatuhumu kufanya mapenzi ya jinsia moja na kuwapiga picha kwa kutumia simu zao.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali, mchungaji huyo alilazimika kupigana na polisi hao kupinga kitendo hicho lakini alizidiwa nguvu na kuvuliwa nguo zote na kubaki na bukta tu.
Taarifa za awali zinasema, siku moja kabla ya tukio hilo, mchungaji huyo alikutana na dereva mmoja wa malori eneo la Njiapanda ya Himo ambaye alisema anafanya biashara ya pumba.
“Kwa maelezo ya mchungaji ni kuwa walipeana simu ili pumba hizo zikipatikana apigiwe. Siku iliyofuata kweli huyo mtu akampigia akisema amepata magunia 150,” mtoa habari wetu alidokeza.
Alisema mtu huyo alimtaka mchungaji afike Bomang’ombe ambako angempeleka kuziona pumba hizo ili kama akiridhika wafanye biashara.
“Yule bwana aliyejifanya ana pumba alimuomba mchungaji amsindikize ili achukue chumba kwa vile siku hiyo angelala hapo Bomang’ombe kusubiri wenzake kutoka Segera.”
Mchungaji na mtu huyo walifuatana hadi katika hoteli moja (jina tunalo) na mtu huyo anayetuhumiwa kupangwa alichukua chumba na mchungaji akaingia kukiona.
“Huyo bwana akaomba akanunue sigara ili akirudi ndiyo waende kuangalia mzigo lakini aliporudi tu, ndipo wakaingia na watu wengine kama watano au sita hivi,” alidokeza mtoa habari wetu.
Watu hao ambao baadaye wanne walibainika kuwa ni polisi, wanadaiwa kuwalazimisha mchungaji na mtu huyo kuvua nguo na kuwarekodi kwa picha wakiwatuhumu kufanya ushoga.
Inadaiwa kwamba walimchukua mchungaji na mtu huyo aliyekuwa naye, wote wakiwa nusu uchi hadi kituo cha Polisi cha Bomang’ombe.
Hata hivyo, badala ya kufungua jalada la uchunguzi, polisi hao wanadaiwa kuwahifadhi watuhumiwa upande wa nyuma ya kituo wakimtaka mchungaji awape fedha.
Inadaiwa kuwa walitaka wapewe Sh10 milioni lakini mchungaji aliwasihi kwamba alikuwa na Sh5 milioni, ambazo aliwapa lakini wakamtaka aongeze zifike Sh6 milioni.
Mchungaji huyo akiwa chini ya ulinzi kuanzia saa 10:30 jioni hadi saa tatu usiku, aliwapigia simu marafiki zake ambao baadaye walimtumia Sh400,000 kwa njia ya simu.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, polisi hao walimchukua mchungaji akiwa na bukta hadi kwa wakala na kumshurutisha awape namba za siri ambazo aliwapa na wao kutoa pesa.
Baada ya kuwapa fedha hizo, walimrudisha hadi nyumbani kwa mmoja wa polisi hao na kumpa nguo zake lakini wakashikilia simu yake kwa sharti la kumrudishia kama tu angewaongezea Sh100,000.
“Baada ya kuachiwa ndiyo siku iliyofuata alitoa taarifa Takukuru ambao walichukua maelezo yake na viongozi wa juu wa Polisi wakajulishwa.”
Katika uchunguzi wa awali uliofanywa siku hiyo kati ya maofisa wa Polisi na Takukuru, ilithibitika kuwa hakuna jalada lolote lililokuwa limefunguliwa dhidi ya mchungaji wala mtu waliyekuwa naye.
Mbali na kutofunguliwa kwa jalada hilo, uchunguzi ulibaini kuwa ni kweli mchungaji huyo alikutwa katika nyumba hiyo ya kulala wageni na kuchukuliwa na polisi na pia muamala wa fedha kwenye mtandao wa simu ulipatikana.
“Wale polisi walikamatwa na kuwekwa mahabusu hadi leo (jana) walikuwa hawajatoka na tayari walishamrejeshea yule mchungaji pesa zake zote Sh5.4 milioni,” mtoa habari adokeza.
Pia, alidokeza kuwa simu yake ambayo polisi waliishikilia hadi atakapokamilisha malipo ya Sh100,000 amerudishiwa kimyakimya ili suala hilo lisije kuwagharimu.
Hata hivyo, mtu aliyekutwa akiwa na mchungaji huyo hajafahamika wala aliko huku taarifa nyingine zikidai huenda naye ni polisi.
Kaimu Kamanda Mkoa wa Kilimanjaro, Koka Moita alisema askari hao wanne wanashikiliwa kwa madai ya kumkamata mtu anayedaiwa kuwa mchungaji na kumtengenezea mazingira hayo.
“Ni kweli tumepata taarifa na tumezifanyia kazi haraka, kinachofuata sasa ni kumpata huyo anayedaiwa kuwa ni mchungaji ili tuweze kumuhoji athibitishe,” alisema.
Inadaiwa kuwa askari hao wamemshawishi mchungaji huyo akubali kuwasamehe na asiandike maelezo ya uhalisia wa tukio, jambo linaloelezwa kwamba amelikubali.

Tuesday, November 22, 2016

UKWELI KUHUSU KIKWETE UWANJA WA NDEGE.

download
JAKAYA KIKWETE.
Rais mstaafu, Jakaya Kikwete, juzi alisafiri nje ya nchi baada ya baadhi ya watu waliokuwa katika ujumbe wake, kukamilisha taratibu ambazo hapo awali zilishindikana na hivyo kuachwa na ndege.
Kikwete na ujumbe wake ambao walikuwa wakielekea nchini Abu Dhabi (Umoja wa Falme za Nchi za Kiarabu – UAE), walishindwa kusafiri Jumamosi iliyopita kwa ndege ya Shirika la Ndege la Emirates, iliyokuwa inaondoka saa 10:30 jioni baada ya baadhi ya wajumbe hao kutokuwa na viza.
Ofisa mmoja wa juu serikalini ambaye jina lake tunalihifadhi kwa sababu maalumu, akizungumza na na gazeti hili jana alisema: “Ni kweli Kikwete na ujumbe wake walishindwa kusafiri siku ya Jumamosi kwa Shirika la Ndege la Emirates baada ya baadhi ya wasaidizi wake kuonekana kuwa na shida kwenye viza.”
Kwa mujibu wa ofisa huyo ambaye alisema hata yeye amefuatilia kwa undani suala hilo, pamoja na shida hiyo kutokea, rais huyo mstaafu aliruhusiwa kusafiri kwa ndege hiyo, ila washauri wakasema ni vyema aliweke sawa jambo hilo ili aweze kuondoka.
“Sio kama alizuiwa, hapana, viza za wasaidizi wake zilikuwa hazijasoma kwenye system (mfumo), baadaye aliruhusiwa ila washauri walisema ni vyema ali-clear (aliweke sawa) kwanza jambo hilo ndipo aondoke.
“Halafu jambo jingine, kama imetokea shida, kwa mtu kama Kikwete kwa hadhi yake anaambiwa akiwa nyumbani, mambo kama yapo sawa sawa ndio anakwenda airport (uwanja wa ndege),” alisema ofisa huyo.


TUHUMA ZA KAJALA KUTEMBEA NA MAKONDA NA MSAMI BABY.

msami
Staa wa Bongo anayetesa kwenye filamu, Kajala Masanja amevunja ukimya na kufunguka kuhusu maneno yanayozagaa mitaani yakimtaja kuwa kwenye uhusiano wa kimapenzi kwa nyakati tofauti na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda na mwanamuziki wa Bongo Fleva, Msamy Baby.
Kwa muda mrefu sasa, minong’ono hiyo imekuwa ikizagaa kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii tangu wakati Makonda akiwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni katika Serikali iliyopita ya Dk. Jakaya Kikwete.
Tetesi za uhusiano wake na RC Makonda, zilianza wakati Makonda (alipokuwa DC wa Kinondoni) akishirikiana na msanii huyo kwenye shindano la kusaka vipaji vya wasanii wa Wilaya ya Kinondoni lililojulikana kama Kinondoni Star Search.
Katika mahojiano na Polisi wa Swaggaz, Kajala alipoulizwa kuhusu madai ya kuwa na uhusiano na Makonda, alijibu kwa kifu sana: “Hapana sijawahi kutoka naye kabisa. Hilo halipo.”
Awali, RC Makonda aliwahi kuzungumzia madai hayo akiwa bado Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, ambapo alisema wabaya wake wa kisiasa wamekuwa wakisaka mbinu za kumchafua kila kukicha.
Makonda, alikwenda mbali zaidi akisema kuwa, propaganda ya kumchafua ilianza tangu wakati wa Bunge Maalum la Katiba, alipokwenda Bungeni na msanii mwingine wa filamu, Yobnesh Yusuf ‘Batuli’, akazushiwa kuwa alitoka naye.
Katika maelezo ya Makonda, alisema anawashangaa wengi wanavyomhusisha kuwa na uhusiano usiofaa na Kajala kwa vile ameshirikiana naye kwenye project hiyo ya kusaka vipaji wakati pia ameshirikiana na wasanii wengi wa kiume.
Kwa Kajala inakuwa mara ya kwanza kuzungumzia hilo katika mahojiano maalum na mwandishi wa Swaggaz.
Kuhusu msanii wa Bongo Fleva, Msami Baby Kajala alisema: “Hata huyo sijawahi kutembea naye, lakini nakiri kwamba ni rafiki yangu wa karibu kama msanii mwenzangu ila hatujawahi kuwa wapenzi hata siku moja.”
SWAGGAZ: Vipi kuhusu picha zilizozagaa kwenye mitandao ya kijamii zikiwaonesha wewe na Msami mkiwa sehemu mbalimbali za starehe?
KAJALA: Kwahiyo nikipiga picha na msanii basi natoka naye?  Mtu unaweza kujisikia kupiga picha na yeyote kwa ajili ya kurusha Insta, kwahiyo ukifanya hivyo tu basi tayari unatoka naye?
Mfano leo (juzi Jumatano) nimepiga picha na Petty Man, kwahiyo nikiweka Insta basi itakuwa Kajala anatoka na Petty. Siyo jambo zuri, nadhani wangekuwa na uhakika kwanza, mimi sijawahi kutembea na Msami.
SWAGGAZ: Ok! Vipi kuhusu uhusiano wako na mzazi mwenzako P Funk kwa sasa?
KAJALA: Kawaida tu! Yeye ana maisha yake na mimi nina yangu, ameoa na mimi niko kivyangu.
SWAGGAZ: Umezungumzia upande wako, vipi kuhusu mwanenu Paula, anawasiliana na baba’ake?
KAJALA: Hapana na hiyo ni kwa sababu mtoto niko naye mimi.
SWAGGAZ: Kwahiyo tangu uachane na P Funk, mtoto hajawahi kwenda kumuona baba yake?
KAJALA: Aliwahi kwenda kipindi fulani na aliishi naye wakati huo, lakini nilipomchukua na kuishi naye hawajawahi kuonana naye tena.
SWAGGAZ: Labda P Funk amewahi kutaka kuonana na mwanaye?
KAJALA: Hapana… nadhani ni kwa kuwa ana watoto wengine anaona wanamtosha huyu hana haja naye. Lakini nisingependa kuendelea kuongelea hayo mambo tena.
SWAGGAZ: Vipi uhusiano wako na mumeo Faraji aliyeko gerezani? Je, huwa unakwenda kumtembelea?
KAJALA: Nilikuwa nakwenda kumwangalia lakini kwa sasa nisiwe muongo, nina muda kidogo kutokana na kazi za hapa na pale, nimejikuta sijaenda kumuona lakini mwanzo nilikuwa nakwenda kila Jumamosi na Jumapili.
SWAGGAZ: Mara ya mwisho kwenda ilikuwa lini?
KAJALA: Mwezi mmoja umepita sasa.
SWAGGAZ: Vipi mipango yako ya kiuhusiano? Maana mumeo yupo jela. Utamsubiri atoke muendelee na uhusiano wenu au unatarajia kuingia kwenye ndoa mpya? Nimekuuliza hili kwa sababu hivi karibuni ulisema unatamani kupata mtoto wa kiume.
KAJALA: Hiyo siwezi kuongelea in public (hadharani) kwa sababu ni maisha yangu binafsi.
SWAGGAZ: Ahsante sana kwa ushirikiano wako.
KAJALA: Nawe pia karibu tena.

MKUTANO WA WANACHAMA WA SIMBA KUFANYIKA DESEMBA 11.

Msemaji wa Simba, Haji Manara
MSEMAJI WA SIMBA, HAJI MANARA.
Uongozi wa klabu ya Simba umeitisha mkutano wa wanachama wa dharura utakaofanyika Desemba 11.
Mkutano huo umeitishwa baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji wa klabu hiyo iliyokaa juzi.
Kwa mujibu wa msemaji wa Simba, Haji Manara, mkutano huo utafanyika kwenye ukumbi wa Bwalo la Maofisa wa Polisi Oysterbay jijini Dar es Salaam.
Alisema Kamati ya Utendaji imetoa baraka zake kupitia ibara ya 22 ya Katiba ya Simba.
“Mkutano huo utakuwa ni mwendelezo wa mkutano wa kawaida uliofanyika Julai 31, 2016,” alisema Manara.
Hata hivyo, taarifa hiyo haijaeleza ajenda za mkutano huo, lakini inadaiwa kuwa huenda ukahusu kuboresha suala la uongozi wa Simba na kuingia katika suala la uwekezaji.

WAZIRI WA ELIMU, NDALICHAKO AJA NA MPYA.

Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako.
WAZIRI WA ELIMU, DR.JOYCE NDALICHAKO.
Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako amesema kuwa baada ya uhakiki wa vyeti vya vifo vilivyowasilishwa na wanafunzi wanaoomba mikopo wakidai kwamba ni yatima, watakaobainika kupeleka vyeti vilivyoghushiwa watafikishwa kwenye vyombo vya sheria.
Hatua hiyo imekuja baada ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) hivi karibuni kubaini uwepo wa baadhi ya wanafunzi ambao wamewasilisha vyeti feki vya vifo vya wazazi wao ili waonekane kama ni watoto yatima, huku wakihitaji kupewa kipaumbele cha kupatiwa mkopo.
Akizungumza katika mkutano wa wadau wa elimu jana Dar es Salaam, Profesa Ndalichako alisema kwa wanafunzi ambao wanatambua kwamba walipeleka vyeti feki vya vifo na ripoti za daktari kuonesha kwamba wana magonjwa mbalimbali ambayo wanastahili kupewa mkopo, wajisalimishe kuepuka usumbufu watakaoupata.
“Timu yetu inaendelea na uhakiki na ripoti itakapokamilika kwa wale wanafunzi watakaobainika wameghushi vyeti vya vifo hilo ni kosa la jinai hivyo watashitakiwa,” alisema Profesa Ndalichako.
Hata hivyo, alitolea mfano Chuo Kikuu cha Mtakatifu Joseph ambacho kilifungiwa Februari mwaka huu kwamba wanafunzi wote waliopelekwa kwenye vyuo mbalimbali walionekana hawana uwezo hivyo walitakiwa kurudia mwaka.


MCHUNGAJI AWAPULIZIA DAWA YA MBU WAUMINI WAKE HUKO AFRIKA KUSINI.

Mchungani wa Afrika kusini ambaye aliwapulizia dawa ya kuua wadudu inayoitwa Doom waumini amelaaniwa vikali.
Katika taarifa aliyoituma kwenye ukurasa wa Facebook, mchungaji aliyejitangaza kama nabii Lethebo Rabalago alidai dawa ya kuua waduduinayojulikana kama Doom inaweza kuwaponya wengi.
Kampuni inayozalisha Doom imeonya juu ya hatari ya kupuliza dawa hiyo watu , huku tume maalum ya serikali ikimtaka yoyote atayeathirika kuwasilisha malalamiko.
Lakini mchungaji huyo ametetea kitendo hicho, alisema kuwa anatumia mbinu zisizo za kawaida kuwaponya watu.
Nchi hiyo imekuwa na wimbila visa ambapo wajumbe wa kanisawamekuwa wakitendewa vitendo visivyo vya kawaida ili kupata tiba.
Katika picha zilizosambazwa kwenye kurasa za Facebook na Twitter, Bwana Rabalago, anayeendesha kanisa la Mountzion General Assembly katika jimbo la Limpopo, anaeonekana akimpulizia dawa ya kuuwawadudu moja kwa moja kwenye macho yake na maeneo mengine mbali mbali ya mwili mbele ya waumini wa kanisa lake.

'Nguvu za Mungu'

Amemueleza mwandishi wa BBC Nomsa Maseko aliyeko mjini Johannesburg kwamba alipuliza dawa hiyo kwenye uso wa mmoja wa wanawake kwasababu alikuwa na maambukizi ya macho na kudai kuwa "yuko sawa kwasababu anaamini nguvu za Mungu".
Pia alidai kuwa dawa hiyo ya Doom inaweza kuponesha saratani na virusi vya HIV vinavyosababisha.
Kampuni inayotengeneza dawa ya Doom kwa nembo ya Tiger inasema kuwa inamsihi s mchungaji aliyejitangazia kuwa ''nabii'' huko Limpopo - Lethebo Rabalogo kuacha kuwapuliza dawa ya wadudu kwenye nyuso za binadamu kama sehemu ya imani ya kuabudu.
Kopo la Doom
''Tunaona tendo hili kuwa kutia hofu kubwa , na tungependa kubainisha wazi kwamba ni hatari kupulizia Doom ama dawa nyingine yoyote ile ya wadudu kwenye macho ya watu''.
''Doom ilitengenezwa kwa ajili ya kuwauwa wadudu wa aina fulani ambao wameonyeshwa kwenye kopo, na maelezo yaliyoandikwa bayana kwenye kopo la Doom yameonya juu hatari na yanapaswa kufuatwa.''
''Kampuni ya Tiger iko katika mchakato wa kuwasiliana na Nabii kumtaka aache kufanya tendo hilo,'' imesema kampuni ya Tiger.
Muumini akipulizwa dawa ya Doom
Lethebo Rabalago akimpulizia muumini Doom

KANYE WEST ALAZWA HOSPITALI.

Kanye West
KANYE WEST.
Mwanamuziki mashuhuri nchini Marekani Kanye West amelazwa hospitalini mjini Los Angeles, vyombo vya habari nchini Marekani vimeripoti.
Msemaji wa polisi amesema kwamba walipokea simu ya kutokea kwa mtafaruku Jumatatu adhuhuri, lakini hawakutaja jina la mwanamuziki huyo.
Baadaye, mtafaruku huo ulidaiwa kuwa tukio la kimatibabu na maafisa wa kutoa huduma ya dharura walifika eneo hilo.
Msemaji wa maafisa wa huduma za dharura wa LA amesema mwanamume ambaye jina lake halikutajwa alipelekwa hospitalini "kufanyiwa uchunguzi zaidi".
"Mwendo wa saa 13:20 majira ya kanda ya pasifiki, idara ya huduma za dharura ya Los Angeles ilipokea ombi la dharura la huduma ya matibabu ambalo halikuelezwa kwa kina," amsemaji huyo alisema.
"Mwanamume mzima, ambaye hali yake ya afya ni thabiti, alipelekwa hospitalini kufanyiwa uchunguzi zaidi."
NBC news wanasema hatua ya kumlaza West imechukuliwa kwa ajili ya afya yake na usalama wake.
Tovuti ya udaku ya TMZ imesema West amepelekwa hospitali kufanyiwa "uchunguzi wa kiakili" na kwamba amekuwa akitafuta matibabu "kwa sababu ya kukosa usingizi sana".
Los Angeles Times imeripoti kwamba kulipigwa simu ya 911 kutoka nyumba ya Kanye West.
West nawawakilishi wake hawajazungumzia tukio hilo.
Mkewe, Kim Kardashian, alitarajiwa kuhudhuria hafla fulani New York Jumatatu, mara yake ya kwanza kutokea hadharani tangu avamiwe na wezi Paris mwezi Oktoba, lakini hakufika.
West alikuwa amefuta tamasha zote zilizokuwa zimesalia kwenye ziara yake ya sasa ya kimuziki.
Alikuwa ameondoka tamasha ya Sacramento ikiwa katikati wikendi.
Alikuwa ameimba nyimbo tatu pekee Jumamosi usiku kabla ya kuanza kuwafokea watu na kushambulia Facebook, Jay Z na Hillary Clinton.
Alimkosoa mkuu wa Facebook Mark Zuckerberg kwa kukosa kumlipa $53m (£42.5m) alipe madeni.
Alisema pia kwamba alikereka sana na hatua ya Jay Z na familia yake kutomtembelea baada ya mkewe kuporwa Paris mwezi Oktoba.