Wednesday, November 2, 2016

WALIOHUSIKA NA KIFO CHA MASHALI WASAKWA.



Wakati mwili wa bondia Thomas Mashali ukitarajiwa kuzikwa leo, watu wanne wanasakwa na polisi wakituhumiwa  kuhusika na kifo chake.
Ndugu wa Mashali, Emmanuel Mashali akiwa nyumbani kwao, Tandale kwa Mtogole, Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam alisema kwamba ndugu yao ataagwa leo saa 7:00 mchana na  kuzikwa jioni kwenye makaburi ya Kinondoni.
“Tunajaribu kuomba kutumia Viwanja vya Leaders Club kufanya shughuli za kuaga, kama itashindika shughuli hiyo itafanyika kwenye Viwanja vya Shule ya Msingi Tandale,” alisema Emmanuel na kuongeza: “Shughuli ya kuaga mwili itaanza saa 7:00 mchana na saa 10:00 jioni tutamuhifadhi ndugu yetu kwenye makaburi ya Kinondoni.”
Akizungumzia kifo  hicho, Emmanuel alisema taarifa za awali walizopata ni kwamba bondia huyo alipigwa na watu kadhaa baada ya kumpigia yowe za mwizi.

MBUNGE AKAMATWA NA BUNDUKI 11.



 Kikosi kazi maalumu kilichoundwa na Serikali kupambana na tatizo sugu la ujangili, kimenasa bunduki 11 ambazo zinasadikiwa kutumika kufanya ujangili na kukamata watu wanne zaidi.
Taarifa zilizopatikana jana zimelidokezea gazeti hili kuwa bunduki hizo zilikamatwa nyumbani kwa mbunge wa CCM (jina tunalihifadhi) ambaye bado anasakwa na kikosi kazi hicho.
Matukio hayo yamekuja siku chache baada ya Rais John Magufuli kutaja jina la mtu anayeitwa Mpemba kuhusika na ujangili kwa muda mrefu wakati alipotembelea ofisi za Wizara ya Maliasili na Utalii na kushuhudia pembe 50 za ndovu zilizokamatwa na watumishi wa wizara hiyo.
Siku hiyo, Rais aliwaambia watu aliowaita “vijana” waendelee na kazi yao ya kukamata wauaji wa tembo, akiwahakikishia kuwa Serikali ipo na kuwataka wasiogope mtu yeyote yule.

LADY JAY DEE KIZIMBANI.

Mahakama ya Wilaya Kinondoni imemtia hatiani mwanamuziki nyota wa kike nchini Judith Wambura (Lady Jay Dee) kwa kutoa maneno ya kashfa dhidi ya Joseph Kusaga na Ruge Mutahaba.
Mahakama hiyo imemuamuru aombe radhi kupitia kwenye chombo cha habari chenye "coverage" pana nchini kote na ikiwezekana duniani.
Katika hati ya madai hayo, mwanamuziki huyo anashtakiwa na viongozi wa Clouds Media Group ambao ni Ruge Mutahaba na Joseph Kusaga kwa kuuchafua uongozi wa kampuni hiyo na viongozi wake kupitia mitandao ya kijamii katika malumbano makali kati ya pande hizo mbili.
Mei 2013, Clouds Media Group na Ruge walimburuza Jay Dee mahakamani kwa kile walichodai kwamba alikuwa akiwatukana kwenye mitandao ya kijamii.

Tuesday, November 1, 2016

FARAJA NYARANDU AHAMASISHA WATANZANIA KUACHA KUMSEMA VIBAYA MISS TANZANIA 2016.

Aliyewahi kuwa Miss Tanzania, Faraja Nyalandu amemkingia kifua mshindi wa mwaka huu Diana Edward akisema hata yeye aliposhinda alizushiwa mambo mengi, lakini anashukuru kwa kuwa yalimjenga.

Katika waraka wake wenye maneno 223 aliouweka kwenye mtandao wa Instagram, mrembo huyo alisema alikaribishwa katika dunia ya umaarufu kwa kashfa lakini kwa msaada wazazi wake alifanikiwa kusimamia malengo yake.

Alimtaka Miss Tanzania afanye anachokiamini na kupuuzia maneno ya watu kwa sababu yanaweza kumtoa katika njia yake.

“Njia ya mafanikio ni ngumu, kwako Miss Tanzania wetu fanya kile unachokiamini, usikubali maneno haya ya watu yakuondoe katika mstari, kwa Watanzania wenzangu tujitahidi kuyaunga mkono yaliyo mazuri, tusibomoe…Tujenge,” alisema.

Akizungumzia ushindi wake, Diana alisema amejipanga kulitumikia vyema hasa kukomesha vitendo vya ukeketaji katika jamii ya Kimasai.


MWANAFUNZI ALIGONGA GARI LA POLISI KWA SABABU YA KUJIPIGA SELFIE.

Mwanafunzi mmoja wa chuo kikuu nchini Marekani aligongesha gari lake kwa lile la polisi, wakati akijipiga picha za selfie huku akiendesha gari.
Miranda Rader mwenye umri wa miaka 19, aligonga gari polisi alipokuwa akimtumia mpenzi wake picha za utupu kupitia kwa mtandao wa Snapchat.
Ajali hiyo iliyotokea eneo la Bryan umbali wa kilomita 160 Kaskazini mwa mji wa Houston, ilisababisha mfuko wa hewa kuchomoka
Mwanafunzi huyo pia alipatikana na chupa ya mvinyo ndani ya gari lake kwa mujibu wa polisi. Hakuna mtu aliyejeruhiwa.
Polisi ambaye gari lake liligongwa alikaribia gari la Bi Rader na kumpata akijaribu kuvaa nguo. Alipoulizwa mbona, alijibu akisema kuwa alikuwa akijipiga picha za selfie za kumtumia mpenzi wake.
Alikamatwa kwa kushukiwa kuendesha gari akiwa mlevi na kuachiliwa kwa dhamana ya dola 2000.

TANZANIA KUSHIRIKI MASHINDANO INDIA.

Timu ya Kabaddi ya wanaume na wanawake ya Tanzania itashiriki Kombe la Dunia la mchezo huo nchini India katika jimbo la Punjab kuanzia keshokutwa hadi Novemba 17 mwaka huu.
Balozi wa India nchini, Sandeep Arya alisema hayo jana jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa watakaoenda nchini India kushiriki Kombe la Kabaddi kutoka Tanzania ni jumla ya watu 34.
Alisema Kabaddi ni mchezo maarufu katika jimbo la Punjab na mikoa mingine ya India na kombe hilo litafanyika katika sehemu tofauti 14 katika jimbo hilo.
Alisema timu 13 zinatoka katika sehemu mbalimbali duniani zitashiriki na kwa upande wa wanaume zinatoka Marekani, Uingereza, Hispania, Dernmark, Iran, Argentina, Canada. Kenya, Sweden, Australia, Tanzania, Sierra Leone na India.
Alisema timu 10 zitashiriki kwa upande wa wanawake ambazo ni Marekani, Uingereza, Dernmark, New Zealand, Mexico, Kenya, Sierra Leone, Australia, Tanzania na India.
Arya alisema Serikali ya India inafurahia kwa timu za Tanzania kushiriki katika sehemu zote mbili yaani timu ya wanawake na wanaume.
Alisema safari na maandalizi ya timu ya Kabaddi yamewezeshwa na kudhaminiwa na Serikali ya Jimbo la Punjab nchini India na kwamba kwa wiki mbili timu hiyo imekuwa ikifundishwa na kufanya mazoezi yake katika kituo cha utamaduni wa India kwa ajili ya maandalizi ya kombe hilo la dunia.
Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohamed Kiganja alisema timu hiyo itaondoka keshokutwa na kuwataka wachezaji kwenda kuiwakilisha vyema Tanzania kwani fursa waliyoipata ni nafasi ya pekee.
Kaimu Mkurugenzi wa Michezo, Alex Kenyenge alisema michezo hiyo ni ya jadi kwa India na kutoa viongozi mbalimbali nchini kuona ni jinsi gani ya kutumia michezo ya jadi iliyopo nchini kwa ajili ya kuitangaza Tanzania katika nyanja mbalimbali.
Kiongozi wa timu ya Tanzania, Abdallah Mustafa alisema timu hiyo ilianza mazoezi na baadaye kuletewa makocha kutoka nchini India na kuahidi kuiwakilisha vyema Tanzania na kuleta ushindi.

UTAFITI:SUMU YA NYOKA NI DAWA YA KUMALIZA UCHUNGU.

NYOKA MWENYE SUMU KALI ZAIDI DUNIANI.

Joka mwenye sumu kali zaidi duniani huenda akawa jibu la kupatikana dawa ya kupunguza uchungu. Hii ni kwa mujibu ya wanasayansi.

Joka anayejulikana kama 'Blue Coral' ndiye mwenye sumu kali zaidi na hupatikana zaizi Kusini Mashariki mwa Bara Asia. Utafiti mpya uliochapishwa kwenye jarida la afya la Toxin umepata joka huyo huwalenga maadui wake ambao husababisha uchungu kwa binadamu.

Wanasayansi wanasema huenda sumu hii ikatumika kutengeneza dawa ya uchungu. Baadhi ya wanyama ambao sumu yao imetumika kutengeneza dawa ni pamoja na konokono wa baharini na bui bui wa sumu.

Wanasayansi sasa wanataka joka huyu kuhifadhiwa hususan baada ya maeneo mengi anakopatikana kugeuzwa kuwa mashamba ya michikichi. Wanasayansi walifanya utafiti wao katika nchi za China, Singapore na Marekani.

Watafiti wanasema japo kwa mwanadamu nyoka huwa adui, lakini wakati huu huenda akawa suluhu la matatizo mengi ya kiafya.