Monday, October 24, 2016

VIJANA MAARUFU WENYE USHAWISHI ZAIDI 2016.

Malala Yousafzai, Jaden Smith, Kylie Jenner, mabinti wa Obama na Chloe Grace Moretz wote kwa mara nyengine wamejumuishwa katika orodha ya vijana walio na ushawishi zaidi mwaka huu katika jarida la Times magazine.
Inatazama athari walio nayo vijana katika vyombo vya habari na katika mitandao.
Orodha hiyo inajumuisha pia waigizaji kutoka vipindi kama Stranger Things, Game of Thrones na Hunger Games.
Ni nyota kutoka sanaa ya musiki, mchezo uanamitindo, sayansi , biashra na siasa.
Malala Yousafzai alipigwa risasi na Taliban mnamo 2012.
Malala Yousafzai
Tangu hapo amekuwa kijana mwenye umri mdogo zaidi kuwahi kushinda tuzo ya Nobel ya amani na kupata kimondo kutajwa kwa jina lake, na kuna taaifa kwamba huenda kukatengenezwa filamu kuhadithia maisha yake.
Akiwa na umri wa miaka 19, Malal amejumuishwa katika orodha hiyo ya vijana wenye ushawishi tangu mwaka 2013 na bado anatetea haki za wasichana kusoma kote duniani.

Mamayao anapendwa kote duniani na baba yao ni rais wa kwanza mweusi Marekani.

Malia na Sasha Obama
Kwahivyo hakuna shinikizo kubwa kwa Sasha na Malia Obama?
Ni vizuri kuona kuwa wanafuata nyayo za wazazi wao, huku Sasha akishirikiana na mamake kuhimiza wanawake wanaelimika Liberia na Mali naye Malia akitarajiwa hivi karibuni kujiunga na chuo kikuu cha Harvard.
Awali wakitazamwa kwa sifa ya watu wawili na dadake Kendall, Kylie Jennermwaka huu amepata sifa peke yake.
Kylie Jenner
Wakati Kendall na Kylie wote wakitokea mara tatu katika orodha hiyo ya vijana walio na ushawishi tangu 2013 - mara moja kila mtu kivyake na mara mbili wakiwa pamoja maarufu "iconic duo," Kendall hakujumuishwa mwaka huu kwasababu ametimiza miaka 20!
Kylie anepeperusha sifa ya jina la familia Jenner kwa kuorodheshwa kwa mara ya nne sasa.
Luka Sabbat na Jaden Smith wanawakilisha wanamitindo wanaume wanaosifika.
Luka Sabbat
Katika mtandao wake wa Instagram anajiita mwanamitindo, mjasiriamali bingwa wa mitindo, na ukampata Tom Ford kukutumia suti , hapana shaka kuhusu sifa anazojipa.
Na Jaden hakuachwa nyuma katika suala la kuwana mtindo wake wa mavazi katika siku za nyuma ikiwemo kuonyesha mitindo ya mavazi ya wanawake ya Louis Vuitton.
Huenda unadhani humjui Maddie Ziegler, lakini ukiiona sura yake utamtambua.
Maddie Ziegler
Anasifika kama mchezaji densi katika kanda ya musiki y ya muimbaji maarufu Sia 'Chandelier na The Greatest', na huambatana na mwanamuziki huyo asiyejulikana sura katika tamasha kuonyesha mfano wake.
Maddie alijumuishwa pia katika orodha ya mwaka 2015 na akiwana miaka 14 tu ndiye kijana zaidi kutambuliwa mwaka huu.

Na orodha haiwezi kukamilika mwaka huu pasi kuwataja wanamichezo nyota.

Simone Biles

Simone Biles na Laurie Hernandez katika mchezo wa gymnastics wamejumuishwa pamoja na waogeleaji Katie Ledecky na mkimbiza wa Syria Yusra Mardini waliong'ara katika mashindnao ya mwaka huu ya Olimpiki.

SHINDANO LA MR & MRS ALBINO LILILOFANYIKA KENYA. TAZAMA ILIVYOKUWA.


Akina dada walioshiriki katika mashindano ya urembo kwa watu wanaoishi na ulemavu wa ngozi ama Albinos jijini Nairobi, Kenya. Tarehe 21 Oktoba 2016.
Mamia walijitokeza kushuhudia maonyesho ya urembo ya Mr na Ms Albino nchini Kenya. kila siku Albino wanakabiliwa na hatari ya kuwawa na viungo vyao vya mwili kuuzwa kutokana na imani za kishirikiana Afrika mashariki na Afrika kusini.

Akina dada walioshiriki katika mashindano ya urembo kwa watu wanaoishi na ulemavu wa ngozi ama Albinos jijini Nairobi, Kenya. Tarehe 21 Oktoba 2016.


WASANII WA BONGO WAAMBULIA PATUPU KWENYE TUZO ZA MTV MAMA.

Tuzo za MTV nchini Afrika Kusini

Wawakilishi wa Tanzania katika tuzo za wanamuziki bora zinazoandaliwa na MTV Africa Music Awards 2016 (MAMA hawakufanikiwa kutwaa tuzo yoyote japokuwa waliweza kushiriki katika vipengele tofauti.
Tuzo hizo zilizotolewa Johannesburg, Afrika Kusini kuamkia jumapili, dalili zilionekana mapema kuwa mbaya kwani Vanessa Mdee aliyekuwa anawania tuzo ya msanii bora wa kike alishindwa baada ya Yemi Alade (Nigeria) kutangazwa mshindi.
Diamond Platinumz aliyekuwa anashindania tuzo ya msanii bora wa mwaka akipambana vikali na Black Coffee, Sauti Sol, Wizkid na Yemi Alade alishuhudia tuzo hiyo akikabidhiwa Wizkid.
Wimbo "Unconditionally Bae" ulioimbwa na Sauti Sol akishirikiana na Alikiba, ambao ulikuwa kwenye kipengele cha wimbo bora wa kushirikishwa haukupata tuzo.
Wimbo huo pia uliambulia patupu katika kipengele cha wimbo bora wa mwaka.
Hata hivyo, Yamoto Band iliyoshiriki katika tuzo hizo katika kipengele cha 'Chaguo la Wasilikizaji' haikufanikiwa kutwaa tuzo hiyo.
Vilevile msanii mwingine kutoka Tanzania aliyeshiriki tuzo hizo maarufu barani Afrika na kushindwa kufurukuta katika medani hiyo ya kimataifa ni Raymond.

CHELSEA 4-0 MAN U

Chelsea 4-0 Man United
Jose Mourinho alifedheheshwa aliporudi katika uwanja wa Stamford Bridge baada ya timu yake ya zamani kuicharaza Manchester United.
The Blues ,ambao walimfuta kazi Jose Mourinho kwa mara ya pili mwaka uliopita waliongoza kunako sekunde ya 30 ya mchezo kuanza baada ya Pedro kupata mwanya katika safu ya ulinzi ya Man United.
Gary Cahill alifunga bao la pili katika kipindi cha pili baada ya United kuruhusu kona iliopigwa na Eden Hazard kudunda katika eneo la hatari la man United.
Chelsea ikikabiliana na Man United katika uwanja wa stamford Bridge
United hawakuonyesha ishara yoyote ya kukomboa mabao hayo ,na hivyobasi wakaongezwa bao la tatu na Eden hazard baada ya mchezaji huyo kupiga mkwaju wa umbalii wa maguu 15.
N'golo Kante aliimwaga safu ya ulinzi ya United na kufunga bao la nne na la mwisho na kuipatia ushindi Chelsea huku ikipanda hadi nafasi ya nne.
United watasalia katika nafasi ya 7 huku pengo kati yao na viongozi wa ligi likiongezeka na kufikia pointi tano.
Wakati huohuo viongozi wa Ligi Manchester City walitoka sare na Southampton katika uwanja wa Etihard.

SIMBA YAONYESHA KUWA SIO TIMU YA MCHEZO MCHEZO.

Simba jana iliendelea kuwapa raha mashabiki wake baada ya kuifunga Toto Africans mabao 3-0 katika mechi ya Ligi Kuu Bara iliyochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru Dar es Salaam.
Ushindi huo umeifanya timu hiyo izidi kujichimbia kileleni mwa msimamo wa ligi ikiwa na pointi 29 katika mechi 11 ilizocheza huku Toto ikibaki mkiani ikiwa na pointi zake nane katika mechi 12.
Mara kadhaa Toto huisumbua Simba zinapokutana, msimu uliopita zilitoka sare katika mechi ya kwanza na timu hiyo ya Mwanza kuibuka na ushindi katika mechi ya marudiano.
Muzammil Yassin ndiye aliyeanza kuamsha shangwe za mashabiki wa Simba baada ya kufunga bao la kuongoza katika dakika ya 43 kwa kuunganisha pasi nzuri ya Fredrick Blagnon.
Toto walicheza mchezo wa kuzuia karibu muda wote wa kipindi cha kwanza, hali iliyosababisha kwenda mapumziko wakiwa nyuma kwa bao hilo moja.
Dakika chache baada ya kuanza kipindi cha pili Blagnon alilazimika kutoka baada ya kuumizwa na beki wa Toto na hivyo nafasi yake kuchukuliwa na Laudit Mavugo.
Mavugo raia wa Burundi hakufanya kosa kwani katika dakika ya 52 aliiandikia Simba bao la pili. Alifunga bao hilo baada ya kupokea pasi safi ya Mohamed Ibrahim ‘Mo’na kuunganisha mpira moja kwa moja nyavuni na kumuacha kipa wa Toto Mussa Kirungi asijue la kufanya.
Muzammil aliwanua tena mashabiki wa Simba katika dakika ya 74 alipofunga bao la tatu kwa kuunganisha mpira wa kona uliochongwa na Said Ndemla na mpira kwenda moja kwa moja wavuni.
Katika mechi nyingine ya ligi iliyochezwa jana kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya wenyeji Prisons walilazimishwa sare ya bao 1-1 na Mbao. Matokeo hayo yanaifanya Prisons kufikisha pointi 16 na Mbao pointi 13 katika msimamo wa ligi hiyo.

WANAOPEWA MIKOPO VYUONI KUBANWA.

Serikali iko katika mkakati wa kuwabana wanafunzi wanaopewa mikopo katika fani za kipaumbele, kutumikia katika utumishi wa umma nchini kwa muda fulani ili kuhakikisha dhamira ya serikali ya kuwapa kipaumbele inatimia.
Fani hizo ni sayansi za tiba na afya, ualimu wa sayansi na hisabati, uhandisi wa viwanda, kilimo, mifugo, mafuta, gesi asilia, sayansi asilia, mabadiliko ya tabianchi, sayansi za ardhi, usanifu majengo na miundombinu.
Hatua hiyo inatokana na serikali kubaini kuwapo wanafunzi wanaosomea fani hizo ili kupata mikopo, lakini baada ya kumaliza hukimbilia kufanya kazi nyingine au nje ya nchi, hivyo upungufu wa wataalamu waliowakusudia kubaki kama ilivyo.
Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Stella Manyanya aliyasema hayo hivi karibuni, alipozungumzia utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu. Alieleza kuwa serikali inafikiria kuwe na utaratibu kwa wanaonufaika na mikopo ya kipaumbele kuingia makubaliano na serikali.
Manyanya alisema kuja na mtazamo na makubaliano hayo, yatakuwa kutumikia katika fani hiyo kwa kipindi fulani; na anapotoka aruhusiwe kwani sasa wapo wanapopangiwa huripoti na kuondoka bila kufanya kazi hizo.
Alisema suala hilo halitakuwa jipya kwani hapo nyuma walikuwa wakibanwa kuwa lazima kufanya kazi angalau kwa miaka mitano serikalini na baadaye ni ruhusa kwenda popote, lakini kwa sasa hawawezi kuwabana wote, lakini lazima kufanya hivyo kwa hao wa kipaumbele.
Alitoa onyo kwa wanafunzi wanaosomea masomo hayo ya kipaumbele, kama hawana wito wa kufanya kazi hizo kuacha.
Alitoa mfano wa walimu wa sayansi ambao serikali inatoa fedha ili kusaidia wanafunzi katika shule za wananchi hususan vijijini, ambako hakuna walimu wa sayansi, hesabu na mengineyo.
Aliwaasa wanafunzi hao kuwa kama nia yao ni kupata mikopo tu, pesa hizo siyo nzuri kwao kwa sasa.
Akizungumzia ulipaji mikopo hiyo, Manyanya alisema wanaboresha sheria ya kukusanya madeni kwa kushirikiana na waajiri.
Alisema serikali itakusanya madeni hata kwa wakopaji ambao wamejiajiri kwa sababu wengi wakimaliza masomo hawafikirii kulipa.
Alisema sasa lazima, wakopaji watambue fedha hizo ni mikopo na lazima kulipa. Alisema kwa wakopaji watakaoajiriwa, wizara inataka mikopo huo kuwa wa kwanza kukatwa kabla ya mingine ili kuepuka kuingiliana na sheria za kazi, zinazotaka mkopaji kuachiwa fedha fulani katika mshahara wake.
Akizungumza wakati wa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa hosteli katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Rais John Magufuli alisema hadi sasa serikali inadai Sh trilioni 2.6 ambazo zilikopeshwa kwa wanufaika mbalimbali wa elimu ya juu, lakini hadi sasa hawajarejesha na hiyo inaleta changamoto kwa waombaji wapya.

MFALME WA MOROCCO AMEWASILI NCHINI NA KITANDA NA MAZULIA YA KIFALME.

Rais John Magufuli akiwa na Mfalme wa Morocco,

 Mfalme Mohammed VI wa Morocco amewasili nchini akiwa na msafara wa ndege tano zilizobeba vifaa vyake, ikiwamo kitanda na mazulia ya kifalme.
Mfalme Mohammed aliwasili jana saa 11:15 jioni akiwa na ujumbe wake wa watu zaidi ya 150, wakitokea nchini Rwanda.
Kabla ya kuwasili kwa ndege yake, zilitangulia ndege mbili ndogo za Morocco zilizokuwa na ujumbe ulioambatana naye.
Awali, Waziri wa Mambo ya Nje, Dk Augustine Mahiga alinukuliwa akisema msafara wa Mfalme huyo ulitanguliwa na ndege mbili zilizobeba vitu mbalimbali kwa ajili ya matumizi yake kwa kipindi chote atakachokuwapo nchini.
“Nadhani mnajua mapokezi ya kifalme yalivyo, wenzetu wanapenda kuandaa wenyewe kila kitu atakachotumia mfalme wao. Ndege mbili zimewasili zikiwa zimebeba vifaa mbalimbali vikiwamo kitanda na mazulia ya kifalme,” alisema Dk Mahiga kabla ya ujio wa Mfalme Mohammed VI.
Mfalme Mohamed VI alipokewa uwanja wa ndege na vikundi mbalimbali vya burudani na raia wa Morocco wanaoishi nchini. Ulinzi uliimarishwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) wa maofisa usalama wa pande zote mbili kwa kuzunguka pande zote za uwanja huo.
Mfalme huyo aliambatana na vyombo vya habari, ikiwamo televisheni maalumu ya familia ya kifalme na televisheni ya Taifa ya Morocco. Kamera za vyombo vya habari vya Morocco na Tanzania zilitawanywa sehemu mbalimbali za uwanja huo ili kupata matangazo ya tukio hilo moja kwa moja.
Baadhi ya wananchi kusimama kando ya barabarani kushuhudia msafara wa kiongozi huyo wa Morocco ulipokuwa ukipita kutokea uwanja wa ndege, walikuwa wakishangilia huku wakipunga mikono.
Kilichomleta  Mfalme Tanzania
Mfalme huyo anatarajiwa kufanya mazungumzo na Rais John Magufuli leo Ikulu jijini Dar es Salaam.
Mambo yatakayojadiliwa na viongozi hao ni uhusiano baina ya nchi zao na Morocco kutafuta uungwaji mkono ili irejee kwenye Umoja wa Afrika (AU).
Mfalme huyo atafanya ziara rasmi ya siku tatu na baadaye ataanza likizo yake na kutumia siku tano zaidi kutembelea vivutio vya utalii.
Serikali za Tanzania na Morocco zitatiliana saini makubaliano mbalimbali ya kibiashara ikiwa ni moja ya mkakati wa nchi hizo kuimarisha uchumi.
Waziri Mahiga alisema lengo la ziara hiyo ni kuanzisha diplomasia ya kiuchumi kwa kuwa Morocco ni moja ya nchi za Afrika zenye maendeleo.
Alisema uhusiano wa Tanzania na Morocco ulianza siku nyingi kupitia ubalozi wa Tanzania uliopo Ufaransa na Ubalozi wa Morocco nchini Kenya. Alisema Serikali ya Morocco imeonyesha nia ya kuanzisha ubalozi wake nchini.
Akizungumzia zaidi kuhusu ujio wa Mfalme huyo, Dk Mahiga alisema Tanzania na Morocco zitatiliana saini mikataba zaidi ya 16 ambayo baadhi yake itakuwa kati ya Serikali Kuu, taasisi na mashirika.
“Hii ni ziara ya kipekee kwa sababu ndiyo mara ya kwanza kwa Mfalme kutembea hapa nchini. Mfalme Mohammed VI ataambatana na wajumbe zaidi ya 150 ambao wengi wao wanatoka familia ya kifalme,” alisema Dk Mahiga.
Waziri huyo alisema ajenda nyingine ya ziara hiyo ni Morocco kuomba kuungwa mkono na Tanzania juu ya azima yake ya kutaka kurejea AU tangu ilipojitoa miaka 32 iliyopita.
Alisema Tanzania inaunga mkono dhamira ya Morocco kurejea AU kwa sababu ni moja ya nchi za Afrika na inahitaji kushirikiana kupitia umoja huo.
Alisema sababu ya Morocco kujitoa kwenye umoja huo ilikuwa ni mgogoro kati ya nchi hiyo na Sahara Magharibi.
“Wao wameona ni fursa kurejea katika Umoja wa Afrika, na sisi hatuoni tatizo katika hilo kwa sababu tunahitaji kushirikiana. Licha ya kutokuwa katika Umoja wa Afrika, Morocco imekuwa ikishiriki shughuli mbalimbali za kimataifa,” alisema.
Hata hivyo, Dk Mahiga alisisitiza kwamba msimamo wa Tanzania katika suala la Sahara Magharibi ni kuitaka Morocco kuiacha huru nchi hiyo kwa sababu zama za ukoloni zilishapita.