Tuesday, November 8, 2016

MAMBA MLA WATU AUAWA.


Mamba mla watu aliyekuwa tishio kwa wakazi wa Kijiji cha Kakobe katika Halmashauri ya Buchosa, Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza, ameuawa na wananchi na kuchunwa ngozi.
Ofisa Mtendaji wa Kata ya Kazunzu, Timotheo Sengerema amesema kuuawa kwa mamba huyo kumewaondolea hofu wakazi hao waliolazimika kusitisha shughuli za uvuvi ndani ya ziwa hilo wakihofia kuuawa na kuliwa.
“Kabla ya kunaswa na kuuawa juzi, mamba huyo alikuwa amewauwa wavuvi watatu walipokuwa kwenye shughuli zao za uvuvi,” amesema Sengerema.
Amesema kazi ya kumtega na kumnasa mamba huyo ilitekelezwa na mmoja wao mwenye ujuzi wa kazi hiyo, Lucas Dambaya kwa ahadi ya kulipwa Sh1 milioni zilizochangwa na wanakiji hao.
“Kazi ya kumtega na kumnasa mamba huyo ambaye wanakijiji  walimchuna ngozi kabla ya kuukabidhi mzoga wake kwa uongozi wa kata ilichukua siku mbili,” amesema Sengerema.
Akizungumza baada ya kumnasa mamba huyo, Dambaya amesema ataendelea kuweka mitego kuwanasa mamba wengine ambao  bado wako kwenye mwalo wa kijiji hicho na kuwataka wakazi hao kuchukua tahadhari wanapofanya shughuli zao ziwani humo.
Mwenyekiti wa kijiji hicho, George Mambile amesema kwa kipindi cha miezi mitatu, wakazi hao walikuwa wakiishi kwa hofu ya kudakwa na mamba huyo mla watu.
Aliushukuru uongozi wa kata kwa kusaidia juhudi za kumkamata na kumuua mamba huyo.

MANENO MATATU YA MWISHO YA SITTA KABLA YA KIFO.

MAREHEMU SAMWEL SITTA
Kabla ya kifo chake Spika wa Bunge mstaafu, Samuel Sitta alisema maneno matatu ya Kiingereza, “that is life” (hayo ndiyo maisha).
Sitta alitamka maneno hayo baada ya kuambiwa na daktari wake kwamba hawezi kupona ugonjwa unaomsumbua.
Akizungumza jana nyumbani kwa marehemu, Benjamin Sitta ambaye ni mtoto wa Sitta alisema baada ya kuzungumza maneno hayo baba yake alifariki dunia.
Alisema baada ya kuelezwa ukweli huo na daktari, baba yake alikubali kwamba huo ndiyo mwisho wa maisha yake hapa duniani.
“Tumepoteza baba na kiongozi ambaye tulimtegemea kwa ushauri wa masuala mbalimbali, tutafuata yale aliyokuwa akituelekeza,” alisema Benjamin ambaye pia ni Meya wa Manispaa ya Kinondoni.
Sitta alifariki dunia saa 10.50 alfajiri kwa saa za Tanzania  wakati akipatiwa matibabu ya saratani ya tezi dume katika Hospitali ya Technical University of Munuch nchini Ujerumani.
Mwezi uliopita mbunge huyo wa zamani wa Urambo Mashariki alirejea nchini akitokea Ujerumani alikokuwa akitibiwa, lakini wiki iliyopita alienda tena kwa ajili ya matibabu zaidi.
Benjamin alisema marehemu atazikwa wilayani Urambo mkoani Tabora, lakini ratiba ya mazishi ingetolewa na ofisi ya Bunge ambayo inaratibu msiba huo.
“Kwa sasa hatujui mwili utawasili nchini lini, utaagwa lini na atazikwa lini ila tunachofahamu ni kuwa atazikwa Urambo,” alisema.
Benjamin alisema masuala mengine yanayohusu familia hiyo yatazungumzwa na mama yake, Magareth Sitta ambaye bado yuko Ujerumani. “Mambo mengine naomba niyaache yatazungumzwa na mama baada ya kurudi nchini, unajua sasa yeye ndiyo nguzo ya familia, hivyo ni vizuri tukamsubiri yeye,” alisema.
Nyumbani kwa marehemu
Watu walikusanyika nyumbani kwa marehemu  Masaki jijini Dar es Salaam tangu saa 2.30 asubuhi jana baada ya taarifa za kifo hicho kusambaa kupitia vyombo vya habari na mitandao ya kijamii.
Miongoni mwa waliofika mapema ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida ambaye alimwelezea Sitta kuwa atakumbukwa kwa mchango mkubwa katika Serikali na chama hicho.
“Sitta alikuwa kiongozi mwadilifu na aliyesimamia haki katika Serikali na CCM, ndiyo maana wakati wa uhai alikuwa mtu wa watu,” alisema Madabida.
Alisema ukiondoa nyadhifa nyingine za uwaziri, uspika na uenyekiti wa Bunge la Katiba, Sitta atakumbukwa kwa kuongoza vizuri Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC).
Mbunge wa zamani wa Tabora Mjini, Aden Rage alisema mafanikio yake katika siasa ulikuwa ni mchango mkubwa alioupata kutoka kwa Sitta.
“Ni pigo kubwa kuondokea na mtu wa aina ya Sitta, busara zake tulizitegemea kupata ushauri, maneno yake yataendelea kuishi vichwani mwetu,” alisema.
Akiungana na Rage, mdogo wa marehemu, Paulo Sitta alisema kaka yake alikuwa mlezi wa familia na ndugu zake kwa ujumla.
“Familia na ndugu zake tumepata pigo kwa kuwa alikuwa mlezi wetu,” alisema.
 Rais Magufuli atuma salamu
Rais John Magufuli amemtumia salamu za rambirambi Spika wa Bunge, Job Ndugai kufuatia kifo cha Sitta.
Rais Magufuli alisema amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa za kifo cha Sitta na kwamba Taifa limempoteza mtu muhimu aliyetoa mchango mkubwa katika uongozi na maendeleo.
“Nitamkumbuka Mzee Sitta kwa uchapakazi wake, uzalendo wake na tabia yake ya kusimamia ukweli katika kipindi chote alichokuwa kiongozi katika ngazi mbalimbali za siasa na Serikali,” alisema.
Rais alitoa pole kwa mke wa marehemu, Magareth Sitta ambaye ni mbunge wa Jimbo la Urambo, familia, wabunge, wananchi wa Urambo na wote walioguswa na msiba huo.
Salamu za CCM
Katika taarifa yake, CCM ilisema imepokea kwa majonzi na simanzi kubwa taarifa za kifo cha Sitta ambaye amewahi kushika nyadhifa mbalimbali za utumishi katika chama na Serikali.
Akiwasilisha salamu za rambirambi za Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kwa Spika Ndugai, Msemaji wa CCM, Christopher ole Sendeka alisema Sitta alikuwa ni kiongozi mchapakazi, mwadilifu na aliyejitambulisha kwa utendaji wenye kufuata falsafa yake ya “kasi na viwango”.

TANESCO KUONGEZA BEI YA UMEME MWAKANI.

Mchakato wa kukusanya maoni ya wadau kwa ajili ya ombi la Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) la kuongeza bei ya nishati hiyo kwa wastani wa asilimia zaidi ya 18.9 ifikapo mwaka 2017, unatarajia kuanza.
Taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya Udhibiti wa wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) imeeleza kuwa Oktoba 4, mamlaka hiyo ilipokea ombi la mabadiliko ya bei ya umeme, hivyo unaandaliwa mkakati wa kukusanya maoni ya wadau wa nishati hiyo.
“Mikutano ya ukusanyaji maoni kuhusu bei inayopendekezwa na Tanesco itaanza Novemba 16 katika mikoa ya Mwanza, Mbeya, Arusha, Dodoma  na kwa Dar es Salaam ni Novemba 23,” inaeleza taarifa hiyo. 
Hatua hiyo imekuja ikiwa ni miezi saba tangu kutangazwa kwa bei mpya ya umeme iliyokuwa na punguzo la asilimia 1.5 hadi 2.4 sanjali na kuondoa tozo ya kuunganishiwa umeme ya Sh5,000 na gharama ya huduma kwa kila mwezi ambayo ilikuwa na Sh5,520.
Mkurugenzi Mkuu wa Tanesco, Felchesmi Mramba alisema shirika hilo limefanya tathmini na kujiridhisha kuwa hakuna hasara itakayopatikana endapo bei hiyo itatumika.

SAMATTA KURUDI KUISAIDIA TAIFA STARS DHIDI YA ZIMBAMBWE.

MBWANA SAMATTA
Nahodha wa timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mbwana Samatta anatarajiwa kuwasili jijini Dar es Salaam kesho Jumatano kujiunga na kikosi cha timu hiyo kwa ajili ya mchezo wa kirafiki dhidi ya Zimbabwe mwishoni mwa wiki.
Kwa mujibu wa taarifa za mitandao ya kijamii za jana, Samatta aliondokana jana Genk, Ubelgiji kupitia Dubai kabla ya kutua jijini Dar es Salaam kesho.
Samatta ameendelea kuonesha umuhimu wa kuichezea Taifa Stars kwa kuitikia mwito wa kocha Charles Boniface Mkwasa licha ya kuwa na majukumu mazito katika klabu yake. Klabu yake hiyo mbali na kushiriki Ligi Kuu ya Ubelgij, pia inashiriki katika Ligi ya Ulaya.
Wachezaji 24 walioitwa na Mkwasa kwa ajili ya mchezo huo wa Novemba 13 mjini Harare, walitarajia kuingia kambini jana.
Wachezaji wa Taifa Stars walioitwa na Mkwasa ni makipa;Deogratius Munishi ‘Dida’ wa Yanga, Said Kipao wa JKT Ruvu na Aishi Manula wa Azam FC.
Mabeki; Erasto Nyoni, David Mwantika wa Azam FC, Michael Aidan wa JKT Ruvu, Mwinyi Hajji, Vincent Andrew wa Yanga, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ wa Simba SC na James Josephat wa Prisons.
Viungo wa kati: Himid Mao wa Azam FC, Mohammed ‘Mo’ Ibrahim, Jonas Mkude na Muzamil Yassin wa Simba SC, wakati viungo wa pembeni ni Abdulrahman Mussa wa Ruvu Shooting, Shizza Kichuya, Jamal Mnyate wa Simba SC na Simon Msuva wa Yanga.
Washambuliaji ni Ibrahim Ajib wa Simba SC, John Bocco wa Azam FC, Elius Maguli wa Oman Club, Thomas Ulimwengu aliyemaliza mkataba wake TP Mazembe ya DRC na kuondoka mwezi uliopita, Omar Mponda wa Ndanda FC na Nahodha Mbwana Samatta wa K.R.C Genk ya Ubelgiji.

MAANDALIZI YA MAZISHI YA SITTA YANAENDELEA.

Maandalizi ya maziko ya Spika mstaafu na mwanasiasa mkongwe wilayani Urambo mkoani Tabora, Samuel Sitta yanaendelea huku ndugu na jamaa wa karibu wakiendelea kuwasili wilayani humo.
Akizungumza nyumbani kwa marehemu mjini Urambo jana, mdogo wake Peter Sitta alisema maandalizi yanaendelea huku wakiendelea kusubiri taarifa za ratiba kutoka kwa Kamati ya Bunge iliyoundwa kuratibu.
Peter alisema awali alipokea taarifa za ambazo zilikuwa zikieleza kuwa hali ya Spika mstaafu si nzuri baada ya kupigiwa simu saa 11:50 alfajiri, na baada ya muda kidogo alipigiwa simu na kufahamishwa kuhusu msiba kutoka huko kwenye matibabu nchini Ujerumani.
Alifafanua kuwa alishtuka sana kwani ni siku chache tu alikuwa anawasiliana naye wakijuliana hali kwani hata yeye hali yake siyo nzuri.
“Nimestushwa sana kwani nimeongea naye kwenye simu akanijulisha afya yake na kusema anaendelea vizuri na matibabu na yeye Samuel alimuuliza kuhusiana na afya yangu kwani hata mimi naumwa pia,” alieleza Peter.
Alieleza kabla ya kifo chake walizungumza kwenye simu baada ya ndugu aliyekuwa akimuuguza kumwambia waongee na ndipo aligundua hali siyo nzuri kwani alikuwa anaongea kwa taabu mno.
Alieleza kuwa kutokana na mazungumzo yale aligundua hali ya kaka yake si nzuri.
Akizungumzia maandalizi ya maziko, alisema hadi sasa haijafahamika kwani kuna Kamati ya Bunge iliyoundwa ambayo imekuwa ikiratibu maandalizi yote na baada ya mwili kuwasili kutokana Ujerumani ndipo kutakuwa na taarifa sahihi za mazishi.
Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Tabora, Hassan Wakasuvi alilieleza gazeti hili kuwa msiba huo, umemshitusha na hakutarajia.
Alisema amepokea kwa masikitiko makubwa kwani chama kimepoteza shujaa wa kisiasa mkoani Tabora na nchi kwa ujumla. Katibu wa CCM Wilaya ya Urambo, Innocent Nanzabar alisema Mkoa wa Tabora na wilaya ya Urambo, wamepoteza mtu muhimu kwao.
Alisema Sitta alifahamika kama ‘chuma cha pua’ hivyo kuzoeleka kwake na jamii itawachukua muda kumsahau. Alisema atakumbukwa kwa mengi kwa jinsi alivyokuwa mpigania haki, mchukia rushwa na kamwe hakupenda uonevu kwa wanyonge na serikali kwa ujumla.
Mama mzazi wa Sitta, Hajjat Zuwena Saidi Fundikira akizungumza kwa masikitiko huku akibubujikwa na machozi, alisema hana cha kusema zaidi ya kulia.
“Nilipokea taarifa hizi kutoka kwa mwanangu Peter John Sitta baada ya kufika nyumbani huku akilia na baada ya kunyamaza ndipo alinieleza kuwa kuna msiba,” alisema na kuongeza kuwa kamwe hatamsahau mtoto wake kwani bila ya marehemu yeye asingeijua ibada ya hija kwani alimpenda katika maisha yake.

WAFUASI WA CHADEMA WAKAA MASAA SABA KUMSUBIRI LEMA KORTINI.

GODBLESS LEMA
Wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wamekaa kwa muda wa saa saba wakimsubiri Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema kufikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha.
Wafuasi hao akiwemo Mwenyekiti wa chama hicho Kanda ya Kaskazini, Amani Golugwa na Mbunge wa Viti Maalumu, Joyce Mukya walikuwa wamekaa kwa saa kadhaa kumsubiri Mbunge huyo.
Walisubiri bila mafanikio huku saa za mahakama zikiwa zinayoyoma.
Lema ambaye hadi jana anasota mahabusu kwa siku ya sita sasa, hata hivyo ilipofika saa saa 8:52 mchana Wakili wa Mbunge Lema, John Mallya alisema inashangaza hadi sasa ni kwa nini Mbunge huyo alikuwa hajafikishwa mahakamani.
Mallya alisema Lema alikamatwa Jumatano iliyopita mkoani Dodoma na kuletwa hadi Arusha na amekaa mahabusu kwa zaidi ya saa 175 na ni kinyume cha haki za binadamu kwani Polisi wanapaswa kukaa na mshitakiwa kwa saa 24.
Alisema wamefungua kesi ya jinai namba 56/2016, ambayo ipo kwa Jaji Salma Magimbi ambaye atasikiliza kesi hiyo kesho asubuhi.
Katika kesi hiyo waliyofungua mahakamani hapo jana ni kutaka Lema aitwe mahakamani ili kesi yake ya msingi anayoshtakiwa nayo isomwe na mshitakiwa apate dhamana.
Pili wamemshtaki Mkuu wa Kituo cha Polisi, Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (RCO), Kamanda wa Polisi (RPC), Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambao pia katika kesi hiyo waliyofungua, wakili Mallya anataka walipwe gharama za usumbufu wa kesi ikiwemo kufuatilia huku na kule ili Lema atoke.
Katibu wa Chadema Kanda ya Kaskazini, Amani Golugwa alidai utawala wa sheria unagandamizwa na sheria imekiukwa.

WATAKAO PERFOM KATIKA TUZO ZA AMERICAN MUSIC AWARDS (AMA).


Katika list ya tuzo kubwa zinazotolewa kwa wanamuziki duniani huwezi kuacha kutaja American Music Awards ambazo hutolewa kila mwaka kwa mastaa wakubwa wa muziki Marekani, tukio hilo ambalo lipo kwenye maandalizi sasa hivi na tuzo hizo kutolewa usiku wa Nov 20 2016 ambazo zitaonyeshwa live  kwenye kituo cha  ABC.
Na tayari list imetoka ya wasanii wa marekani watakaotoa burudani kwenye jukwaa la usiku wa tuzo hizo za AMAs 2016 ambapo watakuwepo wasanii hawa…
lady-gaga-performance-mirrors-billboard-650
LADY GAGA
0f294d5ebb6cca8d6d543eed97fc9670
BRUNO MARS
twenty-one-pilots-final
TWENTY ONE PILOTS

john-legend-chime-for-change-1370130257-article-0
JOHN LEGEND
rs_600x600-161103093953-600-ariana-grande-nicki-minaj-fb-110316
ARIANA GRANDE & NICK MINAJ
maxresdefault
SHAWN MENDEZ
James Bay looking relaxed and happy with his guitar
JAMES BAY
cvv_azlukaetw7p
FIFTH HARMONY
6_green_day
GREEN DAY
chainsmokers-halsey
CHAINSMOKERS & HALSEY
the-weekend-pic
THE WEEKEND.